Demokrasia Yajishambulia Yenyewe Nchini Kenya Kwa Kuzusha Chuki na Mifarakano ya Kikabila

Taarifa kwa Vyombo Vya Habari

Kenya imeangaziwa katika midani za kimataifa baada ya kiongozi wa Muungano wa National Super Alliance (NASA) Raila Odinga kujiapisha kama rais kwenye sherehe iliohudhuriwa na maelfu ya wafuasi wake siku ya Jumanne 30 Januari 2018. Hatua hii inayotajwa kwenda kinyume na katiba ya nchi hasa ikizingatiwa kuwa Uhuru Kenyatta tayari aliapishwa mnamo mwezi Novemba mwaka jana kama rais kufuatia uchaguzi wa Oktoba mwaka jana uliosusiwa na Odinga. Huku tukio hili likiendelea kuzusha mjadala, Harakati ya Kiislamu ya Hizb ut-Tahrir ingependa kusema yafuatayo:-

Sherehe imetoa taswira ya taifa la Kenya jinsi linavyougua maradhi mabaya ya mifarakano ya kikabila na kimaeneo inayotiwa chachu na wanasiasa wake. Licha ya fikra duni za kizalendo na utaifa zinazopigiwa debe mara kwa mara, ni bayana kuwa fikra hizi ni duni na kamwe haziwezi kuleta umoja wa kudumu baina ya watu. Isitoshe, ukabila, utabaka na umaeneo ni mojawepo ya mbinu za wanasiasa wa Kidemokrasia wanazotumia katika kufikia au kubakia kwenye madaraka. Na ukweli huu haushuhudiwi tu hapa Kenya bali hata mataifa makubwa kama vile Marekani kama anavyoonekana Rais Trump hadharani akitoa matamshi ya kiubaguzi. Isitoshe, utawala wake umesheheni wanasiasa wenye sera za kibaguzi na chuki dhidi ya wahamiaji wa kigeni hasa watu wenye asili ya Afrika na Waislamu.

Ni wazi kuwa licha ya mamlaka iliojipa jamii ya Kisekula ya kujitungia katiba na kanuni ni wazi kuwa viongozi wake hawaziheshimu katiba hizo bali huzifuata na kuzikiuka kulingana na maslahi. Huku upande wa serikali ukiitaja hatua ya Raila kuwa ni kinyume na katiba, kwa upande wake, Raila na wafuasi wake nao wanadai kwamba hatua hiyo ilifuata katiba! Vioja havishii hapo; hatua ya serikali ya kuzima vyombo vya habari na kuwatolea vitisho wanahabari kwa kupeperusha hafla ya NASA inakiuka katiba huku vyombo hivyo vikitaja ni haki yao ya kikatiba kupeperusha matangazo. Ndio hivi ndivyo udhaifu wa kanuni za kibinadamu; wanaozitunga na kudai kuzilinda ndio hao hao huzikiuka na kuzivunja.

Twatoa tahadhari kwa Jamii ya Kenya kwa ujumla na hasa ya Kiislamu isitumbukie kwenye mtegano huu wa baina ya NASA na JUBILEE kwani kiasili ni sehemu tu miongoni mwa hila za wanasiasa wa kibepari jinsi wanavyoshindania nafasi ya kukimu na kushibisha matumbo yao huku wao kama walalahoi huambulia patupu!  Ukweli ni kwamba mirengo yote hii huungana na kutengana kwa ajili ya maslahi. Tuliona hivi majuzi jinsi walivyoungana pamoja bungeni kujipa nafasi ya kujizolea kitita cha Shilingi 2.1 Bilioni kujinunulia magari ya kifahari huku gharama za maisha zikiendelea kupanda!

Twatamatisha kwa kukariri kuwa Uislamu pekee ndio ulio na uwezo wa kuzalisha siasa bora na wanasiasa wazuri wenye sera za kuleta ufanisi wa kisiasa, kiuchumi na kijamii kama ilivyoshuhudiwa kwa karne kumi na tatu wakati wa utawala wa Khilafah. Nasi tunaamini, na In Shaa Allah itarudi tena Khilafah hivi karibuni kuongoza tena dunia kwa siasa ya kweli itakayojaza ulimwengu mzima haki na uadilifu.

Shabani Mwalimu

Mwakilishi kwa Vyombo vya Habari Hizb ut-Tahrir Kenya

KUMB: 04 / 1439 H

Jumamosi, 17 Jumadal Uula 1439 H

03/02/2018 M

 

Simu: +254 707458907

Pepe: mediarep@hizb.or.ke