Mikataba Miwili katika Mkataba Mmoja

Ufupisho wa Suali na Jawabu – 2

Suali:

Kijana kutoka Tunisia anataka kununua gari kwa njia ya Halal. Kuna mtu akamuelekeza kwa kampuni fulani inayokodisha gari kwa muda mrefu ambayo pia kuna uwezekano wa kuimiliki baada ya kuisha kwa mkataba wa kukodisha. Ikimaanisha kuwa hii ni mikataba miwili. Je inaruhusiwa?

Jibu:

Mikataba katika Uislamu ni mepesi na iko wazi; na mkataba mmoja hauchanganywi na mktaba mwengine. Kinyume na hali ilivyo katika sheria za kibinadamu.

Mtume (saw) ameharamisha kufungwa kwa mikataba miwili kupitia mkataba mmoja: Mfano mtu kusema nakuuzia nyumba yangu kwa sharti ununue na nyumba yangu nyengine au nakuuzia nyumba yangu na wewe uniuzie nyumba yako. Hilo haliruhusiwi kwa kuwa ni mikataba miwili iliyojumuishwa katika mkataba mmoja, kwani ukisema nakuuzia nyumba yangu ni mkataba wa kwanza na ukisema kwa sharti nami uniuzie nyumba yako ni mkataba wa pili na yote imejumuishwa katika mkataba mmoja. Imesimuliwa kutoka kwa Ahmad Abdul Rahman bin Abdullah bin Masood, kutoka kwa babake, alisema:

“Mtume (saw) ameharamisha mikataba miwili ndani ya mkataba mmoja”

Hivyo kutokana na suali lako, kuna mkataba wa ukodishaji wa gari kwa muda fulani kisha baada ya muda huo unakuwa ni mkataba wa uuzaji wa gari. Makubaliano hayo mawili ya ukodishaji na uuzaji wa gari kati ya mmiliki wa gari na mkodishaji wa gari yako ndani ya mkataba mmoja. Hivyo kwa mujibu wa Hadith hiyo hairuhusiwi.

Ama ungetaka suluhisho, ungelikubaliana na mwenye gari akuuzie gari hilo kwa mkopo, umpe kima cha kuanzia na kima kitakachobakia ukamlipa kidogo kidogo mpaka utakapokamilisha bei muliokubaliana hapo awali, na kwa hali hiyo gari hilo litakuwa ni lako kwa mujibu wa mkataba wa mauziano muliokubaliana awali. Mkataba huu ni mkataba wa mauziano kwa mkopo na unaruhusiwa lakini kwa sharti ya kuwa bei ya uuzaji iwekwe wazi tangu mwanzo wa mkataba ima ni kwa malipo ya mkono kwa mkono au ni malipo ya mkopo wa kulipa kidogo kidogo, na mkataba wa mauziano hufungwa kwa makubaliano ya wahusika.

Kwa hivyo ikiwa wote wamekubaliana juu ya bei fulani, na muuzaji akamuuzia mnununuzi kwa bei ya mkono kwa mkono (cash) na mnunuzi akakubali au akamuuzia kwa bei ya mkopo na mnunuzi akakubali, hili linaruhusiwa maanake ni kujadiliana juu ya bei ya uuzaji sio uuzaji. Kujadiliana kumeruhusiwa. Imesimuliwa na Anas bin Malik kuwa Mtume (saw) aliuza blanketi na bakuli la kunywia maji akasema: “Nani atakaye nunua blanketi na bakuli la kunywia maji?” Bwana mmoja akasema: Nitazinunua kwa Dirham moja. Mtume (saw) akasema: “Nani atakayetoa zaidi ya Dirham? Nani atakayetoa zaidi ya Diraham? Bwana mmoja akakubali kumpa Dirham mbili, Mtume (saw) akamuuzia.

Vilevile, wengi wa wanavyuoni wamesema ya kwamba inaruhusiwa kuuza kitu kwa mkopo kwa bei ya juu kuliko bei yake ya mkono kwa mkono (cash). Imesimuliwa ya kwamba Tawoos, Al-Hakam na Hammad walisema kuwa hakuna makosa ikisemwa: Nakuuzia kwa bei kadhaa ikiwa ni mkono kwa mkono na kwa bei kadhaa ikiwa ni kwa mkopo, naye atachagua moja kati yao. Imam Ali (ra) alisema: Yoyote mwenye kuuza kwa bei mbili; moja ya mkono kwa mkono na nyengine ya mkopo, basi na ataje mojawapo kabla ya kufunga mkataba.

Mwenyezi Mungu ni Mjuzi, Mwenye Hekima.

Link ya Kiengereza: http://hizb-ut-tahrir.info/en/index.php/qestions/jurisprudence-questions/12065.html

Chanzo: Hizb ut Tahrir Kenya

16 Shaaban 1439 Hijria

02 Mei 2018 Miladi