BBI

Katiba za binadamu, msingi wa vurumai,

Na umwangikaji damu, hapa chini ya samai,

Hazina kheri ni sumu, wala mema masilai,

Hazifishi udhalimu, huatwa ubaki hai,

 

Hazitoki kwa Hakimu, Mola Dhul A’lyai,

Mahitaji hazikimu, na adili hazizai,

Wanateseka kaumu, kusaka tonge na chai,

Kukicha hali ni ngumu, kwa rijali na nisai,

 

Demokrasia sanamu, imeleta zai zai,

Ndiyo yenye kuhujumu, milaye Muumba mai,

Ingatukuwa khatamu, ni lilooza papai,

Ifikapo yake zamu, itaminywa kama yai,

 

Hupataje wanadamu, rukhusa kwa zao rai,?

Kujitungia nidhamu, kuhusu hunu uhai,

Sharia ni za Karimu, za viumbe hazifai,

Hata zitiwe pafyumu, au zipigiwe nai,

 

Enyi ndugu isilamu, ni hakika si madai,

Dini yetu imetimu, na nyongeza haitwai,

Kushiriki ni haramu, kuvotiwa BBI,

Kwa khilafa tuhukumu, tuzipate naa’mai,

 

Hapa yatua kalamu, ugani tena sikai,

Haya niloyakalimu, yasiambae ja tai,

Mfumo uisilamu, ni jua la matwilai,

Si khiyari

‘melazimu, imamuna kum’bai,

 

MTUNZI – MOHAMMED BAKARI

 

ALMUFTI

 

MOMBASA – KISAUNI