IMEANGUKA KHILAFAH

Kwa jina lake Jalia, ninaanda kuandika,

Kuhusu hino kadhia, kwetusi ilopitika,

Vigumu nawaambia, kwake kusahaulika,

Ilivundwa kwa hakika, khilafa uthumania,

 

 

Khilafa uthumania, ya mwisho ilochipuka,

Baada ya abasia, na nyenginezo kutuka,

Ilitawala dunia, magharibi masharika,

Kisha ikaja anguka, ndipo sasa tunalia,

 

 

Ndipo sasa tunalia, kwa khilafa kuanguka,

Ja mbuzi twariaria, sitara ishatuvuka,

Madhila yatushukia, wawi wametuzunguka,

Kwa khilafa kuanguka, waisilamu walia,

 

 

Waisilamu walia, izza yao imeuka,

Unyongeni wamengia, haiba ‘mewaepuka,

Wachinjwa pasi hatia, damu yao yamwaika,

Kwa khilafa kuanguka, umma unaangamia,

 

 

Umma unaangamia, dini wamekengeuka,

Kikamilifu sharia, hawafati za Khalika,

Kwa hima wanapapia, kanuni za makhaluka,

Kwa khilafa kuanguka, kiza kimetutandia,

 

 

Kiza kimetutandia, cha mfumo ulozuka,

Ni urasilimalia, wenye shari kupinduka,

Mwitowe demokrasia, mzoga unaonuka,

Kwa khilafa kuanguka, mayatima tumekuwa,

 

 

Mayatima tumekuwa, maishani twakhizika,

Kwa nguvu twatawaliwa,  makafiri vibaka,

Viongozi wetu hawa, waovyo ni  vibaraka,

Kwa khilafa kuanguka, kufari wafurahia,

 

 

Kufari wafurahia, na huku wakitut’eka,

Zaidi walichangia, ngao yetu kuvundika,

Kwa neno mbiu ” huria,” kutugawa matabaka,

Kwa khilafa kuanguka, ni yepi masuulia?

 

 

Ni yepi masuulia?, khifala kiporomoka,

Baia’ kumpatia, Imamu yawajibika,

Dhima kanena nabia, shingoni ametuvika,

Kwa khilafa kuanguka, kurudishwa iwe nia,

 

 

Kurudishwa iwe nia, yetusi ilokitika,

Sirikali asilia, inayovunda mipaka,

Ile ya joghirafia, wakoloni waloweka,

Kwa khilafa kuanguka  natut’ukue hatua,

 

 

Natut’ukue hatua, nafasi yetu kushika,

Tuiregeshe satua, nayo tulioswifika,

Tuwe tunawararua, adui zetu haraka,

Khilafa kutushopoka, huzuni kumetutia,

 

 

Huzuni kumetutia, ngome yetu kubomoka,

Sasa yenda kutimia, karine moya miaka,

Madhilani kusalia, nauza hutujachoka?

Kwa khilafa kuanguka, ni nini twatarajia?

 

 

Ni nini twatarajia, kwa khilafa kuanguka,

Ni hayano maasia, kwa wingi kusambazika,

Matukufu yetu pia, unajisi kupakika,

Kwa khilafa kuanguka, Qur’ani yadhiliwa,

 

 

Qur’ani yadhiliwa, yadunishwa kama taka,

Ijapo yahifadhiwa, kwa myoyo pasi mashaka,

Ni kitabuche Moliwa, kitukufu bila shaka,

Kwa khilafa kuanguka, umoja umepotea,

 

 

Umoja umepotea, wa umma ulotukuka,

Unyonge waulemea, hali yao ni wahaka,

Nani wakuutetea, usizidi kuteseka,

Kwa khilafa kuanguka, ni mswiba na belua,

 

 

Ni mswiba na belua, khilafa imepomoka,

Yabidi kuifufua, ili tupate komboka,

Pamwe na kumkamua, m’bepari mwamerika,

Ngao yetu ni Khilafa, hapano nami natua,

 

 

MTUNZI – MOHAMMED BAKARI 

 

ALMUFTI 

 

MOMBASA – KISAUNI