Tunawapongeza Waislamu kwa Kuwasili kwa Mwezi wa Baraka wa Ramadhan

Taarifa kwa Vyombo vya Habari

Hizb ut Tahrir Kenya inafuraha sana kuwapongeza Waislamu nchini na ulimwengu wote kwa jumla kwa kuwasili kwa mwezi wa baraka wa Ramadhan. Tunapoingia katika mwezi huu wa rehma, toba na kuokolewa na Moto wa Jahannam, tunatoa wito kwa Waislamu matajiri nchini kusaidia kwa kuwapa sadaka ndugu zao na dada zao masikini hususan wale walioathirika na mafuriko.

Tunawakumbusha Waislamu wakati wanapofunga kuhakikisha wanafikia lengo lililotajwa na Allah (swt) ambalo ni uchaMungu, daraja ya juu kabisa kwa Muislamu inayomlazimisha yeye kushikamana na maamrisho ya Allah. Huku hivi leo tukiwa twaishi katika jamii huru ya kisekula ambayo yaitazama dini kama kadhia ya muda tu, twahitaji kupinga mtazamo huu fisidifu na hivyo basi Ramadhan inapasa kuwa mwezi wa Waislamu kuongeza kumkumbuka kwao Allah (swt) kuliko kuwa ni mwezi wa utiifu wa muda tu kwa maagizo Yake. Uislamu ni Dini iliyo kamilifu hivyo basi tunaamrishwa kutabikisha kwa ukamilifu maagizo ya Kiislamu yanayo husiana na mambo ya kisiasa, kijamii na kiuchumi.

Kwa hakika Ramadhan huleta kheri kwa Waislamu wote, lakini hali ya Umma hususan katika ulimwengu wa Kiislamu bado ingali mbaya na ya kutisha huku ukipitia njama ovu za maadui wa Uislamu. Hali nchini Syria inazidi kuzorota kutoka kuwa ni mbaya mpaka kuwa mbaya zaidi huku Amerika na washirika wake ikiwemo Urusi, Iran nk zikiishambulia kwa mabomu mchana na usiku! Waislamu wanaonja mateso haya mabaya katika nyanja zote za maisha kutokana na kukosekana utekelezwaji wa Qur’an katika maisha yao yote. Hivyo basi katika mwezi huu ulioteremka wahyi, tunawakumbusha kusoma Qur’an na kutafakari maana iliyo ndani yake na pia kushikamana imara na mafundisho yake. Wanaposoma Qur’an Tukufu, ndani ya mwezi huu uliofadhiliwa kwa yakini waelewe kuwa mateso haya yatamalizika tu pindi watakapo tabikisha moja ya majukumu ya lazima kupitia kusimamisha tena Khilafah kwa njia (manhaj) ya Utume katika mojawapo ya mataifa makuu ya Waislamu. Khilafah ndio dola pekee itakayo tabikisha sharia ya Quran katika nyanja zote za maisha na kwa hakika itang’oa utawala wa Amerika kwa kuyafurusha majeshi yake yanayoeneza ufisadi ardhini na hususan katika ardhi za Waislamu.

Shabani Mwalimu

Mwakilishi kwa Vyombo vya Habari wa Hizb ut Tahrir Kenya

 

KUMB: 10 / 1439 AH

Jumatano, 30 Sha’ban 1439 H/

16/05/2018 M

Simu: +254 707458907

Pepe: mediarep@hizb.or.ke