Sera za Kirasilimali Zinakuza Kiwango cha Uzazi Jumla (TFR) kuwa Chini

Habari:

Kenya: Kaunti ya Mandera inaongoza kwa kiwango cha uzazi cha juu kikiwa ni 8, ikifuatiwa na Kaunti ya Marsabit kikiwa ni 7, Wajir kikiwa ni 6.7, Turkana kikiwa ni 6.4, Pokot Magharibi kikiwa ni 5.6, Samburu kikiwa ni asilimia 4.9. Kwa upande mwingine, Kaunti ya Nairobi inaongoza kwa kiwango cha uzazi cha chini kikiwa ni 2.5, ikifuatiwa na Kaunti za Nyamira, Kirinyaga na Kiambu zote tatu kila moja kikiwa ni 2.7, Makueni kikiwa ni 2.8, Kaunti za Meru, Tharaka-Nithi, Embu, Mombasa na Nyeri zote tano kila moja kikiwa ni 2.9. Hiyo ni kwa mujibu wa Utafiti wa Kiuchumi wa 2022 uliofanywa na Kitengo cha Takwimu cha Kitaifa cha Kenya. Kwa kuongezea, utafiti huo ulisema kwamba TFR katika ngazi ya kitaifa imeporomoka kutoka watoto 4.8 waliozaliwa mnamo 2009 hadi watoto 3.4 waliozaliwa mnamo 2019. (The Star, Ijumaa, 6 Mei, 2022).

Maoni:

Takwimu hizi mpya ni tone tu katika bahari zinapolinganishwa na takwimu za kimataifa. Takwimu za Kiwango cha Uzazi Jumla (TFR) za kimataifa za 2022 zinaonyesha taswira ya mporomoko wa kijamii na kukithiri kwa kina ufuska katika jamii kama natija ya utekelezaji wa sera za kirasilimali zenye kuchukiza. Viwango vya chini vya TFR vya kutisha vinapatikana zaidi ndani ya nchi nyingi kutoka Ulaya na Asia Mashariki. Baadhi ya mataifa hayo ni Korea Kusini ikiwa TFR yake ni 1, Hong Kong na Singapore kila moja kikiwa na 1.1, Macau na Malta kila moja kikiwa na 1.2, Italia, Uhispania, Moldova, Bosnia na Herzegovina, Saiprasi na Andorra kila moja kikiwa na 1.3, Ujapani, Ugiriki na Uholanzi kila moja kikiwa 1.4 nk. (World Population Review, 2022).

Mapema mnamo Julai 10, 2020, Kitengo cha Marudio cha Idadi ya Watu (PRB) kilitoa ripoti yake ya Idadi ya Watu Duniani mwaka 2020. Sehemu katika ripoti hiyo ilisema kwamba, “ndani ya nchi na maeneo 91-takribani asilimia 45 ya idadi ya watu duniani-viwango jumla vya uzazi viko chini ya kiwango cha wastani cha idadi ya watoto kinachostahili kuchukua nafasi ya kizazi kimoja hadi chengine kando na kuwepo uhamiaji. Na ndani ya nchi na maeneo 21 zikijumuisha nyingi ambazo kwamba zimetaabika kutokana na maafa ya janga la COVID-19, watu wenye umri wa 65 na zaidi wanachukua takribani asilimia 20 ya idadi ya watu.”

Baadhi ya sera za kirasilimali zinazo tambulika kusababisha kuwepo kwa TFR ya chini ni kukuwa kwa miji, kuzidi kujifunga na usawa wa kijinsia, kuzidi kwa idadi ya wanawake katika kupata njia za kupanga uzazi, wanawake kutafuta fursa za elimu na ajira duniani. Kwa upande mwingine, sababu zinazotajwa kuwepo kwa TFR ya juu ni juhudi chache za tawala za kidemokrasia katika kufanyiakazi sera zinazopigia debe usawa wa kijinsia, wanawake kupata fursa za kutumia njia za kupanga uzazi, elimu na ajira miongoni mwa nyinginezo.

Sababu hizo hapo juu ni za kweli kuhusiana na kwamba zimevuliwa kutokamana na nidhamu ya kijamii huria ambayo kwamba kipaumbele chake ni uhuru wa kibinafsi. Kwa kuongezea, thamani ya wanadamu katika Urasilimali inazingatiwa kutokamana na mtizamo wa mchango wao katika uzalishaji wa kiuchumi. Hivyo basi, sio jambo la kushangaza kushuhudia ufuska wa kupindukia katika jamii kwa jina la kuwa wanawake wanatafuta kujiwezesha na kiujumla kujikomboa kiuchumi. Karne ya 21 inazingatiwa kuwa ndio karne ya ushindani wa papatu baina ya jinsia kwa ajili ya fursa chache zilizopo za ajira.  Hakika, fursa ni chache kwa kuwa upo ukiritimba wa rasilimali (utajiri) unaofanywa na warasilimali wachache kupitia makampuni yao ambayo yanazidhibiti na kuziendesha kisiri serikali zote za kidemokrasia duniani.

Leo kuzaa au kuwa na watoto kunazingatiwa kuwa ni mzigo wa kijamii na kiuchumi kwa kuwa watu wengi wanataka kuishi maisha yao kama ndege wanao hama kutoka kiota hiki hadi kile eti wanafurahia uhuru wao wa kibinafsi usiokuwa na mipaka. Hivyo basi, watu wanashiriki katika uzinifu pasi na wasiwasi wa kuhesabiwa bora tu wawe wameridhiana. Miito hadaifu imepenya katika jamii kama vile ‘mavazi yangu, chaguo langu, mwili wangu, chaguo langu, uzazi wangu, chaguo langu,’ nk. Vurumai za kijamii zimeshamiri kila siku na lau pana watoto basi hutumika kwa ajili ya lipizi la kifedha! Viungo vya familia vimeangamia huku watoto wakikabiliwa na ukatili wa kijamii!

Ni muhimu kutambua kwamba HAKUNA taifa duniani kote, ambalo halitaabiki kutokamana na janga la TFR kuwa chini. Ni moja miongoni mwa majanga yanayokabili mataifa pasi na kuzingatia kuwa yapo katika unaoitwa ulimwengu wa kwanza, pili au watatu.  Katika urasilimali thamani ya wanawake msingi wake ni kutumiwa kimwili katika uzalishaji wa kiuchumi. Hayo ni kinyume na Uislamu, ambapo wanawake wanatambuliwa kuwa ni tunu kutokana na dori yao ya kulea vizazi vyenye shaksiyya ya Kiislamu vya wanachuoni, watawala na wanajeshi kwa njia ya Mwenyezi Mungu (swt) na Mtume Wake (saw). Katika Khilafah inayotarajiwa kusimamishwa kwa njia ya Utume, tunu ya wanawake itarudishwa mahali pale kama ilivyokuwa hapo awali kabla kuangushwa kwa Khilafah mnamo 28 Rajab 1342 H (3 Machi 1924 M). InshaAllah.

Imeandikwa kwa ajili ya Afisi Kuu ya Habari ya Hizb ut Tahrir na

Ali Nassoro Ali

Mwanachama wa Afisi Kuu ya Habari ya Hizb ut Tahrir