Kifungo cha Watoto Wahamiaji chaTrump Chadhihirisha Umbile la Kinyama Lisilokubalika la Nidhamu ya Kitaifa ya Kidemokrasia ya Amerika

Taarifa kwa Vyombo vya Habari

Chini ya sera ovu ya uhamiaji ya ‘kutokuwa na hata chembe ya uvumilivu’ ya Raisi wa Amerika, takriban watoto 2000, wengine wao wakiwa na umri mdogo wa miaka 4 au 5, ni miongoni mwa wale walioorodheshwa kama ‘wahamiaji haramu’, wametenganishwa kwa nguvu kutoka kwa wazazi wao katika mpaka wa Amerika na Mexico katika kipindi cha wiki sita pekee. Wametiwa ndani ya vibanda vya seng’enge katika vituo vya vizuizi, ambavyo hali zake zimesifiwa kuwa ‘mithili ya gereza’. Mojawapo ya vituo hivi vya wahamiaji katika jimbo la Texas kimepewa lakabu ya La Perrera, “kibanda cha mbwa”, ambamo watoto wanalala chini sakafuni juu ya magodoro membamba na makaratasi ndio blanketi zao. Kanda ya sauti ya watoto walioathirika kimawazo na kulia imepatikana, wakililia wazazi wao. Idara zimetangaza mipango ya kujenga mahema yatakayobeba mamia zaidi ya watoto katika jangwa la Texas ambako viwango vya joto kawaida hufikia nyuzi 40.

Licha ya kudhihirishwa hasira na shutuma kutoka kwa wanasiasa wa Amerika, vyombo vya habari vya kimagharibi na hata wake za waliokuwa maraisi dhidi ya unyama wa Trump kwa watoto hawa wahamiaji, wamepuuzia kimakusudi ukweli kwamba ni nidhamu katili ya kitaifa ya kidemokrasia ya Amerika ndiyo iliyoruhusu kanuni ya Flores dhidi ya kutoa makao kwa uhamiaji ambayo nyuma ilipitishwa na bunge la Congress inayohalalisha kwa kuruhusu idara kuwatenganisha watoto kutoka kwa wazazi wao kwa njia hii ya kinyama. Hivyo basi sera hii ‘isiyokubalika’ sio tu natija ya ukatili wa Raisi pekee. Ni mojawapo ya matunda yaliyooza ya nidhamu ‘isiyokubalika’ ya kidemokrasia ya Amerika inayofungua mlango kwa sera ovu kama hii inayopitishwa na kuidhinishwa na sheria, kwa msingi uchukizao wa ubaguzi wa kitaifa wa wale wanaotawala. Ni dalili gani zaidi inayohitajika kudhihirisha unyama huu wazi, upuzi na ubaguzi wazi wa rangi wa utaifa na muundo wa siasa za kitaifa za dola, unaodunisha, kudhalilisha, kunyanyasa na kutesa watoto wa wale ambao haja yao ni kutafuta tu maisha bora ya kiuchumi kwao na familia zao, lakini ikatokea kuwa wamezaliwa katika ardhi tofauti? Trump hajutii kuwaita wahamiaji kama wanaoleta “vifo na uharibifu” nchini na kama “wezi na wauwaji”, akijua kuwa hakuna hatua za kisheria atakazochukuliwa kutokana na matamshi yake maovu, ya uchochezi, na ya ubaguzi wa rangi. Ule ukweli kuwa dola yenye uchumi imara ulimwenguni na ardhi kubwa, kuwakataza majirani zake kuingia, kutokana na kuwatazama kama mzigo kwa uchumi, inaeleza kwa kinywa kipana kuhusu roho mbaya, na umbile la uchoyo la mfumo wa kimada wa kirasilimali na siasa zake za dola za kitaifa zilizofeli kwa wanadamu. Tumeshuhudia pia unyama sawa na huu na misimamo ya kikatili dhidi ya uhamiaji iliyochukuliwa na mataifa ya kirasilimali ya Ulaya, Australia na ulimwengu wa Kiislamu – ambako watu wenye fadhaiko wanaokimbia mateso na unyama wamenyimwa hifadhi, wamefanyiwa idhilali ya hali ya juu na kuregeshwa kwenda kufa katika maeneo ya vita au kutelekezwa kufa maji baharini, yote ikiwa tu ni kwa sababu ni watu wenye utaifa tofauti na ardhi wanakotafuta hifadhi.

Kinyume na nidhamu ya kitaifa ya kidemokrasia ya Amerika inayoonesha ulimwengu kuwa ndio kigingi cha unyama, Khilafah kwa njia ya Utume inapinga fahamu ya mipaka katili ya kitaifa pamoja na utaifa au uasabiya wa kila aina. Badala yake, itawakaribisha wale wanaotoka katika ardhi nyenginezo kuja kuishi chini ya utawala wake ili waonje uadilifu wa hali ya juu na ufanisi wa mfumo wa Allah (swt). Hii ndio sababu Khilafah ya nyuma ilitoa hifadhi kwa zaidi ya Mayahudi wakimbizi 150,000 waliokuwa wakikimbia mateso kutoka kwa Manaswara wakati wa uchunguzi wa Kihispania na kuwawezesha kunawiri chini ya utawala wa Kiislamu. Khalifah wa zama hizo, Sultan Bayezid II pia alituma maagizo katika kila sehemu ya dola kwamba wakimbizi hao wapokewe. Katika tangazo lake, Sultan huyo aliwaambia Mayahudi kuwa kuwachunga wao ni amri ya Allah, kuona kuwa wako na chakula na kuwaweka chini ya ulinzi wake. Yote haya yanaonesha tofauti baina ya nidhamu ambayo lengo lake ni kumnyanyua mwanadamu kutokana na unyanyasaji, kinyume na nidhamu ambayo ufafanuzi wake wa ubora ni kuulazimisha juu ya wanadamu!

إِنَّ اللّهَ يَأْمُرُ بِالْعَدْلِ وَالإِحْسَانِ وَإِيتَاء ذِي الْقُرْبَى وَيَنْهَى عَنِ الْفَحْشَاء وَالْمُنكَرِ وَالْبَغْيِ يَعِظُكُمْ لَعَلَّكُمْ تَذَكَّرُونَ﴿

“Hakika Allah anaamrisha kufanya uadilifu, na ihsani, na kuwapa jamaa wa karibu; na anakataza uchafu (zinaa), na uovu, na dhulma. Anakupeni mawaidha ili mupate kukumbuka.” [16: 90]

Dkt. Nazreen Nawaz

Mkurugenzi wa Kitengo cha Wanawake katika Afisi Kuu ya Habari ya Hizb ut Tahrir

 

H.  10  Shawwal 1439 Na: 1439 AH / 028
M.  Jumapili, 24 Juni 2018