Ni Yapi Yanayo Endelea Nchini Saudi Arabia? Amerika Inasimama Msimamo Upi Kuhusiana Nayo?

 Bismillah Al-Rahman Al-Raheem
(Imetafsiriwa)

Swali:

Mnamo tarehe 19/11/2017, tovuti ya Al-Mudun ilifichua kuwa kampeni dhidi ya ufisadi inayoenedelea nchini Saudi Arabia imeanza kuathiri huduma ya jeshi. (Afisa wa Kisaudi, anayeifahamu vyema kampeni hii dhidi ya ufisadi nchini Saudi Arabia, alifichua kukamatwa kwa maafisa 14 wastaafu wa kijeshi waliokuwa wakifanya kazi katika Wizara ya Ulinzi, na maafisa wawili wa kitengo cha ulinzi wa kitaifa, kwa kushukiwa kuhusika katika kesi za ufisadi za kandarasi za kifedha) (Al-Mudun: 19/11/2017), na kukamatwa huku kulianza tangu tarehe 4/11/2017 ambapo Mfalme Salman bin Abdul Aziz alipounda kamati ya kupambana na ufisadi chini ya uongozi wa mfalme mtarajiwa Mohammed bin Salman, huku ikihusisha pia idadi ya mawaziri wa zamani na viongozi wa kibiashara na kusitishwa kwa akaunti zao na za jamaa zao wa karibu, (shirika la wanahabari wa kigeni (Reuters) lilinukuu – kamati ya chunguzi wa ufisadi imesitisha akaunti ya benki ya amiri Mohammed bin Nayef, mfalme mtarajiwa aliyeondoshwa mamlakani na ambaye ni mmoja wa watu maarufu zaidi katika familia tawala ya Saudi, na akaunti za jamaa zake wa karibu. Bin Nayef ndiye aliyekuwa mfalme mtarajiwa kabla ya mfalme aliyeko sasa kumbadilisha na kumueka mwanawe, Mohammad bin Salman na kisha kamati hiyo kuwakamata ma-Amiri 11…) (Shirika la habari la BBC idhaa ya Kiarabu, 8/11/2017). Ni yapi yanayo endelea nchini Saudi Arabia? Ni upi msimamo wa Amerika kuhusiana nayo?

Jibu:

Ili jibu lipate kueleweka kwa uwazi tutaelezea kwa mukhtasari kuhusu familia ya Saud na ushirikiano wao kisha tuendelee na jibu:

  1. Familia ya Al-Saud imeshirikiana na kafiri mkoloni tangu uasi wao wa kwanza dhidi ya Dola ya Kiuthmani kama dola ya Kiislamu. Walishambulia na kutia uchochezi kwa usaidizi wa wakoloni wa Kiingereza dhidi ya Kuwait mnamo 1788, Makkah na Madina mnamo 1803-1804 na kuzivamia biladi hizi. Waliishambulia Dimishki mnamo 1810, huku wakaazi wake wakiihami kwa ujasiri mkubwa, lakini hatimaye wakaidhibiti Aleppo na miji mengine. Walipatiliza fursa ya kulitumia dhehebu la Wahhabi katika kazi yao, na Waingereza wakawatumia kuishambulia dola ya Kiislamu. Lakini baadaye, dola ya Kiislamu ilifaulu kumaliza uasi huu ulioongozwa na Al Saudi mnamo 1818, kupitia gavana wa Wilaya ya Misri, Muhammad Ali.

Walisukumwa tena na Uingereza kuanzia mwishoni mwa karne ya 19, mnamo 1891, lakini dola ya Kiuthmani ikawashinda nguvu. Uingereza ikawasukuma tena mnamo 1901, na ukuruba wao na Uingereza na usaidizi wa Uingereza kwao ukafichuka.

Waingereza walipatiliza fursa ya udhaifu wa dola ya Kiuthmani na kuingia kwake katika Vita vya Kwanza vya Dunia ili kuutia nguvu msimamo wa familia ya Saud dhidi ya watu wa Najd na Hijaz waliopigana dhidi yao vita vya muda mrefu mpaka Wasaudi walipoweza kuwashinda na kudhibiti maeneo haya na kisha kutangaza ufalme wao mnamo 1932, kwa usaidizi wa Uingereza dola iliyokuwa ikiongoza zama hizo.

Lakini baada ya Amerika kugundua mafuta nchini humo na kutokwa na mate kwa utajiri wao, walianza kutafuta ushawishi wa kisiasa nchini humo. Hili lilidhihirika kwa kuneemeka kwa watu wa familia hii ya kifalme, hususan miongoni mwa warithi wa ufalme huo watoto wa Abdul Aziz, mfalme muasisi, baada ya kifo chake mnamo 1953. Hivyo basi, mzozo kati ya Uingereza na Amerika ukaanza nchini humo.
2- Hivi sasa kibaraka wa Amerika Salman ameweza kuchukua udhibiti, na kuanza mchakato wa kuuza rasilimali za vibaraka wa Uingereza na wafuasi wao. Mtangulizi wake, aliyekuwa mfalme mwenda zake Abdallah, alihusishwa na Waingereza, na akajaribu kujishughulisha na vibaraka wa Uingereza waliokuwa mamlakani kabla ya kifo chake, lakini ada ya familia yake ya upokezaji mamlaka ilimlazimu kumteua Salman bin Abdul Aziz kama mfalme mtarajiwa na kudumisha utulivu katika familia hiyo ya kifalme. Alijua kwamba kaka yake ni kibaraka wa Waamerika; hivyo basi, akabuni cheo cha mrithi wa kiti hicho cha ufalme ili kuhakikisha kuwa athari ya Uingereza, na akamteua kaka yake na kibaraka mwenzake, Muqrin bin Abdul Aziz, katika cheo hicho cha mrithi mwenza. Ili awe kibaraka wa Uingereza, kana kwamba aliona mbele kuwa Salman ni mkongwe na mgonjwa na hivyo basi kumpa fursa Muqrin kuchukua udhibiti hadi kifo cha Salman na kisha Muqrin kuchukua utawala kwa njia nyepesi. Kama ilivyo tokea wakati Fahad alipokuwa mzee na mgonjwa, na yeye, yaani Abdallah akawa wakati huo mfalme mtarajiwa na kuchukua udhibiti, na Fahad alipokufa mnamo 2005, Abdullah akachukua mamlaka. Lakini kilicho tokea baada ya kifo cha Abdallah mwanzoni mwa 2015 na kuchukua hatamu za uongozi kwa Salman haikuwa kwa hesabu za Abdullah; Salman alimtimua “Muqrin” kutoka kwa wadhifa wake na kumteua Muhammad bin Nayef kama mfalme mtarajiwa na mwanawe, Muhammad, kama naibu mfalme mtarajiwa, na kuwatimua wengi walioteuliwa na Abdullah katika nyadhifa nyeti, na kuanza kutilia nguvu mamlaka ya mwanawe, Muhammad, hadi mnamo 21/6/2017 alipomuondoa Muhammad bin Nayef kutoka kwa wadhifa wake na kumtangaza mwanawe kama mfalme mtarajiwa na kutomteua yeyote mwengine kuwa naibu mfalme mtarajiwa.
3- Tulitaja katika jibu la swali la mnamo 25/1/2015 baada ya Salma kuchukua mamlaka baada ya kifo cha Abdullah yafuatayo: mfalme aliyeko sasa, Salman, anatoka katika fani ya kijeshi, na hivyo basi, inatarajiwa kuwa athari ya Kiamerika imekita mizizi katika utawala wake, Abdullah alitambua hili, na kwa sababu hii alibuni ada mpya nchini Saudi Arabia, nayo ni, kuwa mfalme atateua sio tu mfalme mtarajiwa wake bali pia naibu mfalme mtarajiwa. Alitambua kuwa Salman bin Abdul Aziz anafuata Amerika, na kinyume na ada maarufu kuwa mfalme huteua mfalme mtarajiwa wake, mfalme Abdullah akateua naibu mfalme mtarajiwa kugawanya njia kati ya mfalme mpya, na kumteua mfalme mtarajiwa kutoka kwa vibaraka wa Amerika. Kwa hivyo, mfalme mwenda zake, Abdullah, alimteua kwa mapema naibu mfalme mtarajiwa; alimteua Muqrin kuwa mfalme mtarajiwa wa Salman bin Abdul Aziz kwa lengo tulilo tangulia kulitaja. Katika jibu la swali hilo, tulitaja: Muqrin anatambulika kwa mahusiano yake na Waingereza. Alisomea huko na kufuzu kutoka katika shule maarufu ya Cranwell nchini Uingereza. Aliaminiwa na mfalme mwenda zake Abdullah, na hata kuwa miongoni mwa washirika wake wa karibu. Ili kusitisha kuendelea kwa silsila ya vibaraka wa Amerika baada ya Salman bin Abdul Aziz, mfalme huyo mwenda zake akabuni wadhifa wa naibu mfalme mtarajiwa. Mfalme Abdullah aliidhinisha uteuzi huu kupitia kutoa azimio kuzuia kuondolewa kwa naibu mfalme mtarajiwa. Lakini hesabu za Waingereza zilikoseka kwa sababu Salman alikiuka mkataba huo pamoja na kanuni na ada, na kumuondoa Muqrin na kumteua kwa muda Muhammad bin Nayef na kisha kumtenga na kumfanya mwanawe, Muhammad, kuwa mfalme mtarajiwa na kumkabidhi mamlaka na nyadhifa kadhaa muhimu ili awe mtawala pekee.

4- Pindi baada ya mfalme Salman kutangaza kuunda kamati kuu ya kupambana na ufisadi mnamo 4/11/2017 chini ya uenyekiti wa mwanawe, Muhammad, mfalme mtarajiwa. Vikosi vya usalama viliwatia nguvuni Maamiri 11 na mawaziri 4 wa sasa na mara moja akawatimua afisini, ishara kuwa hili si jambo la kawaida na halina uhusiano na vita dhidi ya ufisadi, lakini ni sawia na yale yanayotokea katika mapinduzi, ambapo ukamataji hufanyika na utimuliwaji afisini na kushtakiwa hufanywa mara moja. Vile vile, ukamataji ulihusisha idadi kubwa ya mawaziri wa zamani na viongozi wa kibiashara na kufungiwa akaunti zao na akaunti za jamaa zao wa karibu, hii pia ikiwemo kufungiwa kwa zaidi ya akaunti 1700 za benki, ambapo haya “yanaongezeka kila saa” (Shirika la Reuters). Na miongoni mwa wale waliofungiwa akaunti zao ni akaunti ya Muhammad bin Nayef, aliye timuliwa wadhifa wake wa mfalme mtarajiwa hivi majuzi, pamoja na akaunti za idadi kadhaa ya jamaa zake wa karibu. Shirika hilo liliripoti, “Idara za Saudi zilisema zimewaweka kizuizini washukiwa zaidi, kwa sababu ya ukiukaji sheria, ambao ni watu wa familia ya kifalme na wafanyi biashara vilevile wakiwemo mameneja na maafisa kutoka ngazi za chini.” Hili linathibitisha kuwa mchakato huu ni sawia na yale yanayofanyika katika mapinduzi. Kampeni hii ilipanuliwa kujumuisha watoto wa mfalme aliyetangulia; waziri wa ulinzi wa kitaifa, Meteb bin Abdullah (pia hutamkwa Miteb/Mutaib), nguvu ya pili kuu sambamba na jeshi, na kakake Turki bin Abdullah, aliyekuwa Amiri wa Riyadh.

Na Metab bin Abdullah alifuzu kwa cheo cha luteni kutoka katika chuo cha mafunzo ya kijeshi cha kifalme cha Sandhurst ambacho ni chuo cha mafunzo cha jeshi la Uingereza ambapo kwa kawaida ni vibaraka wa Uingereza pekee ambao hupata mafunzo na kufuzu chuoni humo, naye alitanguliwa na wengi katika maamiri wa eneo la Ghuba na wafalme na maamiri wa Jordan. Kakake Turki bin Abdullah ana shahada ya uzamili (masters) katika sayansi na mikakati ya kijeshi kutoka chuo kikuu cha Uingereza cha Wales. Alifutwa kazi na Salman baada ya kuwa afisini kama Amiri wa Riyadh. Inaonekana kuwa Amerika imepata njia ya kuwango’a vibaraka wa Uingereza kupitia mashtaka ya ufisadi. Kwa hivyo, imemuagiza Salman na mwanawe, Muhammad, kutabanni njia ya kufanya hivyo, kama zifanyavyo serikali nyingi sasa kuwango’a wapinzani kwa kuwatuhumu kwa ufisadi. Hususan kwa kuwa watawala wote katika serikali hizi zilizo tangulia na zilizofuata zimechafuka kwa ufisadi, rushwa, wizi wa mali ya umma, mapendeleo kwa wale walio karibu yao na miradi inayo kiuka sheria, kuchukua haki za wengine, dhulma kwa raia na utumizi mbaya wa mamlaka yao kupata yale ambayo wao na washirika wao wanayo yataka. Na ni ufisadi upi mkubwa zaidi kushinda kuacha kufuata sheria za Allah na kufuata sheria za nchi za kikafiri za kikoloni?

5- Tumeona usaidizi wa Amerika katika kampeni hii na kwa wale wanaoitekeleza. Raisi wa Amerika kwenye ujumbe wake katika mtandao wa Twitter mnamo 6/11/2017, alisema: “Nina imani kubwa kwa Mfalme Salman na mfalme mtarajiwa wa Saudi Arabia, wanajua barabara kile wanachokifanya”, akafuatiza na ujumbe mwengine: “Baadhi ya wale wanaokabiliana nao kwa ukali wamekuwa wakiikamua nchi yao kwa miaka mingi.” Shirika la habari la Kisaudi lilisema kwamba “mfalme mnamo Jumapili 5/11/2017 alifanya maongezi ya simu na raisi wa Amerika katikati ya matukio haya ya kisiasa na kiusalama ndani ya Ufalme huo, na kujadiliana kuhusu ushirikiano baina ya nchi mbili hizi katika nyanja tofauti tofauti na njia za kuziboresha.” Trump alizungumza na mfalme wa Saudia kuhusu kuiorodhesha kampuni ya Aramco katika soko la hisa la New York na kwamba angeshukuru endapo Riyadh itaorodhesha hisa za kampuni hiyo katika soko la ubadilishanaji la New York.

Mfalme naye akajibu kwamba watafanya utafiti juu ya utumiaji wa soko la ubadilishanaji wa hisa la Amerika,” Shirika la wanahabari wa kigeni la Reuters liliripoti haya mnamo 4/11/2017. “Tunaendelea kuzishajiisha idara za Saudia kuendelea kuwashtaki watu wanaoamini kuwa maafisa wafisadi; na tunatarajia kuwa watafanya hivyo kwa njia ya haki na uwazi,” Msemaji wa wizara ya kigeni ya Amerika Heather Nauert alinukuliwa akisema haya na shirika la habari la Reuters mnamo 7/11/2017. Hii yaonyesha kuwa Amerika inasimama nyuma ya kampeni hii na kuiunga mkono na kuielekeza dhidi ya watu wasio takikana na Amerika au wale ambao inashuku utiifu wao kwa Amerika au ni vibaraka wa Uingereza au hawaridhishwi na yanayojiri na yale ambayo mfalme na mwanawe ambaye ni mfalme mtarajiwa wanayo yafanya ya kuiuza nchi kwa Waamerika kwa mwendo wa kasi.

6- Kinacho thibitisha kuwa kampeni hii ni kampeni halisi ya kisiasa ni kuwa kamati hiyo (ya kupambana na ufisadi) mara moja ilianza kazi yake ya kukamata na kufunga akaunti za watu muhimu serikalini, na watu wa familia hiyo ya kifalme na jamaa za mfalme…Hivyo basi, ni kampeni halisi ya kisiasa, na wala haina uhusiano wowote na ufisadi wala mageuzi, hususan kwa kuwa Salman na mwanawe wenyewe wamezama ndani ya ufisadi na ufujaji wa mali ya umma, ikiwemo ruzuku iliyopewa Amerika ya dola bilioni 460. Sauti ya taarifa iliyopeperushwa na shirika la habari la Saudia ilikuwa ya ukali kana kwamba ililenga kuzigonga nguvu zenye msemo zinazopinga serikali; ilielezwa katika taarifa hiyo, “Kuundwa kwa kamati hii ilitokana na kuwepo unyanyasaji unaofanywa na watu wenye nafsi dhaifu wanaoyapa kipaumbele maslahi yao binafsi juu ya maslahi ya umma, na kuiba pesa za umma pasi na kupata kizuizi cha kinafsiya kutoka katika dini, akhlaqi au utaifa. Wakitumia fursa ya athari waliyo nayo na mamlaka waliyo kabidhiwa katika kufuja na kubadhirisha pesa, huku wakitumia njia kadha wa kadha kuficha vitendo vyao hivi vya kufedhehesha. Na kisha ukamataji huu ukakolezwa mara moja baada ya kuundwa kwa kamati hii mnamo 4/11/2017.

7- Kisha baada ya hapo mnamo 5/11/2017, ilitangaza kuwa Naibu wa Gavana wa eneo la Asir, Mansur bin Muqrin, pamoja na baadhi ya maafisa waliuwawa katika ajali ya ndege aina ya helikopta, na kuna shaka kuwa tukio hili linahusiana na ung’oaji huu. Hususan kwa kuwa amiri huyu ni mtoto wa Muqrin, aliyekuwa mfalme mtarajiwa aliye timuliwa na Salman baada ya Salman kuchukua mamlaka moja kwa moja. Idadi ya walio kizuizini imezidi mamia. Sa’ud Al-Mu’jab, mkuu wa sheria wa Saudia, alisema: “Watu 208 wameombwa wafike kuhojiwa kuhusiana na uchunguzi wa ufisadi, saba kati yao wameachiliwa huru kwa kukosekana ushahidi wa kutosha… Thamani ya kipesa ya matendo haya ya miongo mingi yamehusisha viwango vikubwa vya pesa zilizo badhirishwa na kufujwa na thamani ya kihakika ya viwango hivi huenda ikazidi dola bilioni 100 za Kiamerika kulingana na yale yaliyojitokeza katika uchunguzi wa mwanzo” (Al-Hayat, 9/11/2017). Upekuzi huu umekuwa ukifanywa kwa miongo kadhaa ndani ya stakabadhi za jamaa wa familia ya kifalme na wenye msemo katika utawala, inayo ashiria kuwa kadhia hii ni ung’oaji tu wa watu mamlakani na athari katika utawala ambao huenda ukageuza mambo kwa mfalme mtarajiwa mwana wa Salman endapo hatatekeleza ung’oaji huu maalum ili kuleta mabadiliko yasiyo ya kawaida kwa serikali na kwa jamii nchini humo, juu ya kuwa amepanda ngazi ya kuwa mfalme mtarajiwa wakati hastahiki kuchukua wadhifa huo kuambatana na ada za familia hiyo…

8- Hivyo basi, yanayo endelea nchini Saudi Arabia chini ya kinachoitwa kampeni dhidi ya ufisadi ni kuwakata Waingereza na kuwazuia kupanga njama ya jaribio la mapinduzi au, pengine, dhidi ya Mfalme Salman na mwanawe mfalme mtarajiwa, pamoja na kufaulisha ugurishaji salama wa utawala kwenda kwa mfalme mtarajiwa ili asiwepo yeyote wa kumpinga; kwa kuwa mwana huyu amejitolea kibinafsi kutumikia maslahi ya Amerika pasi na kuwepo utesi wa kindani hata kama ni kwa jamaa yake wa karibu! Na kutoka kwa wapinzani wote wa kinje, hususan Uingereza, ili kudumisha athari iwe pekee kwa Amerika kisiwani humo… Hivyo basi, uhaini huu haugawanyiki

 (وَأَنَّ اللَّهَ لَا يَهْدِي كَيْدَ الْخَائِنِينَ)
“… na kwamba Allah haziongoi hila za makhaini” [Yusuf: 52].

9- Mwisho, kila siku inapopita inathibitika kuwa hakuna kheri ndani ya serikali zote hizi: si kwa serikali ya familia ya Saud wala serikali ya Iran wala kwa serikali yoyote iliyoko katika biladi za Kiislamu wala kwa wale wanaowafuata na kutii maamrisho yao. Zinaendeshwa na makafiri wakoloni wanaofanya kazi kuendeleza ukoloni wao juu yetu na kufuja utajiri wetu kwa uongozi huo. Hivyo basi, hakuna budi kipaumbele cha mwanzo katika kazi kiwe ni kubadilisha sura halali ya serikali hizi, zilizo egemea matakwa ya kafiri mkoloni.

(وَلَا تَرْكَنُوا إِلَى الَّذِينَ ظَلَمُوا فَتَمَسَّكُمُ النَّارُ وَمَا لَكُمْ مِنْ دُونِ اللَّهِ مِنْ أَوْلِيَاءَ ثُمَّ لَا تُنْصَرُونَ)
“Wala musiwategemee wale wanaodhulumu, usije ukakuguseni Moto. Wala nyinyi hamna walinzi badala ya Allah, wala tena hamtasaidiwa”
[Hud: 113].

Kisha kuondoa muozo wote huu na ufisadi uliosababishwa na nchi za kikoloni, ima Amerika au Uingereza au nyenginezo, kwani ukafiri ni mila moja katika uadui wake dhidi ya Uislamu na Waislamu… Na wote wanaofuata nchi hizi au wanaoshirikiana nao kwa njia ya moja kwa moja au isiyo ya moja kwa moja na kutabikisha mipango yao na miradi yao na kudumisha nidhamu zao za kisekula ni wahalifu na wataadhibiwa kwa fedheha.

 (سَيُصِيبُ الَّذِينَ أَجْرَمُوا صَغَارٌ عِنْدَ اللَّهِ وَعَذَابٌ شَدِيدٌ بِمَا كَانُوا يَمْكُرُونَ)
“Itawafikia hao walio kosa udhalili na adhabu kali kutoka kwa Allah kwa sababu ya vitimbi walivyo kuwa wakivifanya.” [Al-An’am: 124].

Suluhisho hili la matatizo yetu na wala hakuna suluhisho jengine: ni kung’olewa kwa serikali hizi na kuasisiwa Khilafah Rashidah katika njia ya Utume… hata kama litakataliwa na wenye shaka na kuonekana kama jambo gumu na walegevu, lakini ikhlasi kwa Allah (swt) katika kazi hii na ukweli katika kumuiga Mtume (saw) italifanya jambo lililo mbali kuja karibuni kwa idhini Yake (swt),

(وَيَقُولُونَ مَتَى هُوَ قُلْ عَسَى أَنْ يَكُونَ قَرِيبًا)
“Watakutikisia vichwa vyao, na watasema: Lini hayo? Sema: A’saa yakawa karibu!”
[Al-Isra’: 51]

Hapo ndipo ahadi ya Allah itakapotimia.

(وَيَوْمَئِذٍ يَفْرَحُ الْمُؤْمِنُونَ * بِنَصْرِ اللَّهِ يَنْصُرُ مَنْ يَشَاءُ وَهُوَ الْعَزِيزُ الرَّحِيمُ)
“Na siku hiyo Waumini watafurahi. Kwa nusra ya Allah, humnusuru amtakaye Naye ndiye Mwenye nguvu Mwenye kurehemu”
[Ar-Rum: 4-5]

2 Rabii’ I 1439 H
20/11/2017 M