Mgogoro wa Zimbabwe ni Njama ya Uingereza ya Kubadilisha Vibaraka Wake na Kudumisha Hali Halisi

Habari:

Zimbabwe inakabiliwa na mgogoro wa kisiasa wa chama tawala cha Zanu-PF, kama maonyesho ya umma juu ya ni nani anaye tarajiwa zaidi kumrithi Raisi Robert Mugabe. Kikwazo kilichopo kwa sasa ni baina ya kundi la vijana, wenye utiifu kwa mkewe, Grace Mugabe, na waliokuwa wapiganaji wa ukombozi, wenye utiifu kwa Emmerson Mnangagwa, makamu wa raisi aliyefutwa kazi wiki iliyopita. [Aljazeera]

Maoni:

Eneo la Kusini mwa Rhodesia lililo badilishwa jina kuwa Zimbabwe mnamo 18 Aprili 1980 baada ya kupewa uhuru bandia na bwana wake mkoloni Uingereza. Lakini ukweli ni kuwa Uingereza kama dola yenye nguvu zaidi duniani ambayo ilishuhudia hasara kubwa baada ya Vita vya Pili vya Dunia iliyo ifanya kurekebisha sera yake ya kigeni kupitia wadadisi wake wa kina. Matokeo yake yakawa ni kuchora mapendekezo ya kuhakikisha kuwa Uingereza ina makinika moja kwa moja katika kudumisha msimamo wake wa kiulimwengu nyumbani huku ikisimamia koloni zake kwa njia isiyo ya moja kwa moja kwa kupitia vibaraka wake alio wachagua. Hii itatoa fursa kwa Uingereza kuficha njama zao nyuma ya pazia huku uhakika ukiwa wao ndio wenye amri juu ya vibaraka hao watiifu wanao tawala kwa baraka na muongozo wao. Hii ikimaanisha kuwa sera za koloni zao za kindani na kinje zitaundwa kutokana na matakwa ya bwana Uingereza.

Ama kuhusu Zimbabwe, Waingereza walimchagua Robert Gabriel Mugabe anayetoka katika kabila kubwa zaidi la Shona nchini Zimbabwe ambaye walimpa mafunzo na kumuajiri katika taasisi zao ndani ya nchi pamoja na ng’ambo kama mwalimu. Kisha baadaye kumnyanyua daraja kuwa kama mwanamapinduzi na mwanasiasa kwa kumuhukumu kifungo cha miaka 10 gerezani kuanzia 1964 mpaka 1974. Wakati wa kuachiliwa kwake alikimbilia Msumbiji na kuasisi uongozi wake na kusimamia chama cha ZANU ambacho alikuwa mwenyekiti wake kwa miaka mitano kuanzia 1975 – 1980.

Kisha baadaye baada ya kufanywa ‘uchaguzi mkuu’ wa kisanii na Mugabe kushinda Februari 1980; Waingereza walimtawaza Mugabe kuwa Waziri Mkuu wa kwanza wa Zimbabwe mnamo 18 Aprili 1980 ambapo alitawala kwa muda wa miaka saba. Mugabe alianza kumhudumia bwana wake kwa ikhlasi na kwa bidii; kwa mfano kati ya mwaka wa 1982 na 1985 aliuvunja vunja upinzani ulioongozwa na chama cha Zimbambwe African Peoples Union (ZAPU). Hii ni baada ya wito wa Mugabe wa kulingania maridhiano kati ya makabila kushindwa kusitisha kuzorota kwa mahusiano kati ya makabila na kukua kwa chuki dhidi ya wazungu. Zaidi ya watu 10,000 waliuwawa na jeshi la Mugabe wengi wao wakiwa ni raia wa kabila la Ndebele walio kuwa wakiongozwa na Joshua Mqabuko Nyongolo Nkomo kama kiongozi na mwanzilishi wa chama cha ZAPU ambaye pia anatoka katika kabila la Ndebele (Kalanga).

Bwana mkoloni akapanga njama za kumtuza Mugabe kwa kazi yake nzuri. Mnamo 22 Disemba 1987, wakaviunganisha vyama vya ZANU na ZAPU na kuunda chama cha Zimbabwe African National Union – Patriotic Front. Waanzilishi wa chama cha ZANU-PF walikuwa ni Mugabe na Joshua; na wenyekiti walikuwa Emmerson Mnangagwa na Phelekezela Mphoko. Mnamo 31 Disemba 1987, Robert Mugabe akatawazwa kuwa raisi wa kwanza wa Zimbabwe na ili kuhakikisha kuwa mpinzani wake Joshua Nkomo anawekwa chini ya uangalizi, akafanywa kama makamu wa raisi asiye na mamlaka yoyote.

Mugabe amekuwa mamlakani kwa muda wa miaka 37 mtawalia akimhudumia Mmagharibi ‘bwana mkoloni’ kwa ustadi; kile ambacho kimekuwa kikiumisha kichwa Uingereza ni nani miongoni mwa vibaraka wake wengi atakaye mrithi kibaraka wao. Ikizingatiwa kuwa watu wanataka mabadiliko kutokana na maendeleo duni ya kijamii na ya kiuchumi. Mwito wa mabadiliko una ongozwa na Morgan Tsvangirai kinara wa chama cha Movement for Democratic Change – Tsvangirai. Morgan Tsvangirai alikuwa kibaraka wa Uingereza mwanzoni lakini kisha kuhamia kambi ya Amerika. Muingereza ana yakini kuwa watadumisha hali halisi lakini kilicho muhimu zaidi kwao ni kudandia hamasa za watu na hamu ya mabadiliko iso muelekeo na kuleta mabadiliko ya kisanii kupitia kumuunga mkono mmoja wa vibaraka wake kupanda ngazi ya utawala.

Bila ya kujali iwapo Grace Mugabe au Emmerson Mnangagwa ndiye atakaye panda ngazi ya utawala hilo kwao haliwashughulishi wala sio kipao mbele. Hivyo basi, yale yanayo shuhudiwa nchini Zimbabwe katika mgogoro uliopo sasa ni njama ya Uingereza kuwahadaa watu kuwa kuna mabadiliko ya kiutawala ilhali ukweli ni kuwa, yanayo endelea ni mabadiliko tu ya sura. Watu watakao panda ngazi ya utawala watadumisha mfumo ule ule wa kirasilimali na nidhamu zake ovu ikiwemo demokrasia na nidhamu ya kijamii na kiuchumi itakayo endelea kufuja mali ya umma na kuongeza zaidi viwango vya ufisadi wa kijamii na kiuchumi.

Hali halisi ili thibitishwa na taarifa zifuatazo:

  1. Jeshi la Zimbabwe (Zimbabwe Defence Forces), ambalo mshahara wake unatoka Uingereza lilipo sema mnamo 15 Novemba 2017, “Kwa watu wetu pamoja na ulimwengu nje ya mipaka yetu, tungependa kuweka wazi kuwa haya sio mapinduzi ya kijeshi kwa serikali. Kile ambacho jeshi la Zimbabwe kinafanya kwa uhalisia ni kutuliza hali ya uzorotaji wa kisiasa, kijamii na kiuchumi nchini mwetu, ambayo ikiwa haitashughulikiwa huenda ikasababisha mzozo wa kivita” iliyo somwa na Meja Jenerali SB Moyo [Aljazeera: http://www.aljazeera.com/news/2017/11/zimbabwe-military-statement-seizing-power-171115061457199.html]
  2. Umoja wa Mataifa, ambao uko chini ya ushawishi wa dola za kimagharibi hususan Amerika, “Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres alitoa wito kwa pande zote nchini Zimbabwe kuonyesha “kujizuia” baada ya jeshi la nchi hiyo kuchukua mamlaka na raisi Robert Mugabe kusema kuwa yuko chini ya kifungo cha nyumbani. Guterres anafuatilia hali hiyo na “kuomba utulivu, kusitisha ghasia na kujizuia,” akasema msemaji wa Umoja wa Mataifa Farhan Haq [Daily Nation: http://www.nation.co.ke/news/africa/United-Nations-African-Union-reacts/1066-4188994-ssay0/index.html]
  3. Muungano wa Afrika ni mkono mwengine wa dola za kimagharibi hususan Uingereza, “hali ya utulivu ya kikatiba iregeshwe haraka iwezekanavyo na kutoa wito kwa wadau wote kuonyesha uwajibikaji na kujizuia,” sehemu ya taarifa ya Muungano wa Afrika. [Gazeti la Daily Nation: http://www.nation.co.ke/news/africa/United-Nations-African-Union-reacts/1066-4188994-ssay0/index.html]

Ali Nassoro

Mwanachama wa Hizb ut Tahrir Kenya