Tunajifunza Nini Kutokana na Changamoto ya INEOS 1:59?

Mnamo Jumatatu, 6 Mei 2019, Eliud Kipchoge alitangaza duniani kwamba atajipa changamoto ya kukimbia mbio ndefu chini ya saa mbili. Litakuwa ni jaribio lake la pili baada ya jaribio la kwanza huko mji wa Monza, Italia ambalo alikamilisha kwa saa 2 na sekunde 25. Kwa kuongezea, alisema, “Nataka kufutilia mbali fikra kuwa mwanadamu ana kikomo,” na kuongeza “Hakuna vizuizi unapojiamini na kujaribu unachofanya.” Udhamini wa changamoto hiyo ulijulikana kama INEOS 1:59 –Hakuna Mwanadamu aliye na Kikomo na kudhaminiwa na mwanzilishi na mwenyekiti wa INEOS, Sir Jim Ratcliffe.

Kufikia Jumamosi, 12 Oktoba 2019 changamoto hiyo iliandaliwa huko Vienna na dunia ilishuhudia mshindi wa mbio ndefu za Dunia na Olympic Elliud Kipchoge aliweza kukata utepe kwa kufaulu changamoto hiyo kwa kuweka rekodi ya saa 1 dakika 59 na sekunde 40. Ndani ya mbio hizo za kilomita 42 chini ya saa mbili, Eliud alidumu kukamilisha kila kilomita ndani ya dakika 2 na sekunde 50. Baada ya kukamilisha changamoto hiyo Kipchoge alisema, “Nahisi furaha. Imechukua miaka 65 kwa mwanadamu kuweka historia katika riadha. Baada ya Roger Bannister, imechukua miaka 65. Nina furaha kuwa mwanadamu aliyekimbia chini ya saa mbili. Hakuna mwanadamu aliye na kikomo…”

Kwa kuliangalia makini tukio la Changamoto ya INEOS 1:59, linaweka wazi wadhamini wengi na kampeni kubwa za kibiashara. Ama kuhusu kudhamini kisingizio cha majukumu ya mashirika kwa mujtama, makampuni makubwa ya kirasilimali ya eneo na kimataifa yalikuja na miradi mikubwa katika tukio hilo. NIKE ilidhamini viatu vya Kipchoge, INEOS ilidhamini tukio zima. Safaricom ilitoa bando za bure kwa watu ili kutizama moja kwa moja kupitia YouTube na wengineo. Ilikuwa wazi kwa makampuni ya kirasilimali yalikuwepo kupatiliza tukio hilo kwa maslahi yao binafsi kwa kuwa kampuni hizi huwa hazionekani katika masuala ya mujtama ambayo hayana manufaa ya kimada kama vile mkasa wa Likoni feri uliotokea Septemba 2019 ndani ya Kenya!

Ama kuhusu matangazo ya soko, mbio hizo zilitangazwa na kupeperushwa moja kwa moja duniani kote kwa maelfu ya washangiliaji waliohudhuria kutizama moja kwa moja hivyo kuifanya kuwa moja ya matukio makubwa duniani. Hakika, hili limekuwa ni mfano wa namna vyombo vya habari vya leo vilivyo na nguvu. Wengi katika watu walikuwa hawana haja wala walikuwa hawalijui tukio hilo la riadha. Lakini kwa nguvu za vyombo vya habari dunia yote ilitekwa. Walitumia miito kama, ‘Nani anayeweka kikomo? Mbio dhidi ya wakati, Mbio ndefu za Kipchoge ni sawa na kushuka katika mwezi, Mbio za kihistoria’ vyombo vya habari na makampuni duniani yalipelekea kuweko na dhana na mizaha mingi hivyo kupelekea kuzidi kwa mauzo pamoja na kuzidisha soko la bidhaa zao. Kwa hakika, dunia ya makampuni ikapatiliza tukio hilo na kujaza mifuko yao ilhali wengi wa watu wamebakia masikini pasina kutambua.

Ama kuhusu kauli mbiu ya tukio kwamba ‘Mwanadamu hana Kikomo’. Ni kauli mbiu ya urongo kwa kuwa inajulikana kwamba mwanadamu anapojiangalia, anatambua kwamba ameumbwa na hivyo basi ana vikomo vingi na lau angelikuwa hana kikomo angelijiumba mwenyewe; hilo sio kweli. Kwa kuzingatia kuwa changamoto ilifungwa katika 1:59 na Eliud Kipchoge alikamilisha 1:59:40 inathibitisha wazi kwamba ana kikomo na hivyo pia wanadamu wengine. Mwanadamu amepewa changamoto kujituma na katika kufanya hivyo inasemekana yupo katika changamoto ya kujua ukomo wake.

Abu Leila